kiongozi wa harakati ya Ansarullah ya Yemen, Abdul-Malik al-Houthi, amesema kundi hilo liko tayari kwa hatua yoyote ya kuongezeka kwa mzozo katika eneo la Mashariki ya Kati na linaendelea kuwa katika uratibu kamili na washirika wake wa kikanda.
Akihutubia taifa kupitia televisheni ya Al-Masirah, Al-Houthi alisema kuwa Yemen iko tayari kukabiliana na maendeleo yoyote yanayoweza kujitokeza katika hali ya sasa ya usalama na kisiasa. Alisisitiza kuwa kuna ushirikiano wa karibu kati ya Ansarullah na makundi ya kile kinachojulikana kama "Mhili wa Muqawama" kuhusu matukio yanayoendelea nchini Lebanon na Palestina.
Kiongozi huyo pia alizionya nchi za eneo hilo dhidi ya kile alichodai kuwa ni juhudi za Marekani za kuzivuta katika vita vinavyolenga kuitumikia Israel. Alieleza kuwa Mashariki ya Kati inapitia kipindi nyeti kinachohitaji uelewa mkubwa, umakini na uwajibikaji kutoka kwa mataifa na wananchi wake.
Al-Houthi aliishutumu Israel kwa kile alichokiita uhalifu wa wazi dhidi ya wananchi wa Palestina na Lebanon, akidai kuwa Tel Aviv inaendeleza sera za uchokozi zinazolenga kupanua mzozo katika eneo hilo.
Wakati huo huo, Wizara ya Mambo ya Nje ya serikali ya Ansarullah nchini Yemen ilitangaza kuunga mkono msimamo wa Hezbollah kuhusu makubaliano yaliyofikiwa kati ya serikali ya Lebanon na Israel. Katika taarifa yake, wizara hiyo ilisema kuwa njia ya muqawama ndiyo yenye uwezo mkubwa wa kuzuia mashambulizi ya Israel na kumaliza uwepo wa majeshi yake katika ardhi ya Lebanon.
Kauli hizo zinatolewa katika kipindi ambacho mvutano wa kikanda umeendelea kuongezeka, huku juhudi za kidiplomasia zikiendelea kutafuta suluhu ya kudumu ya migogoro inayolikumba eneo la Mashariki ya Kati.
Your Comment